12 July 2012

Baba Mzazi Wa Mwanamuziki Diamond Aibuka-Soma ALICHOSEMA


BABA mzazi wa nyota wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul Juma ‘Diamond’, (pichani) Abdul Juma ameibuka ambapo mbali na tukio hilo pia amenena mambo mazito kuhusu mwanaye huyo huku akimsukumia tuhuma nzito mama mtu, Amani linaanika kila kitu.
ASAKWA PANDE ZOTE ZA DAR
Awali lilitangulia zoezi la kumsaka baba Diamond katika pande zote za Jiji la Dar es Salaam ili kumsikia alichonacho moyoni kuhusu mafanikio ya mwanaye huku taarifa za mahali anapoishi zikipotoshwa na watoa habari wetu.
Wapo waliosema mzee huyo anaishi Kibamba, wengine Mbagala, pia wapo waliodai anakaa Manzese au Magomeni, jijini Dar es Salaam.
Timu ya mapaparazi wa Amani ilizama kazini kikamilifu ikiapa kumnasa mzazi huyo popote alipo na hatimaye Julai 2, 2012 saa saba mchana ilifanikiwa kupabamba nyumbani kwake, Magomeni Kagera, jijini Dar es Salaam lakini mwenyewe hakuwepo.
Ziliachwa salamu za utambulisho kwa jirani mmoja ili atakaporudi mzee huyo amtaarifu kuwa mapaparazi watarudi siku nyingine.
Julai 7, 2012 saa tano asubuhi mapaparazi wetu walitinga nyumbani hapo na kumkuta mzee huyo akisema alipata salamu na alikuwa akisubiri ujio huo, hivyo akawa amejiibua mwenyewe.
AANZA KWA KUANIKA HISTORIA KWA UFUPI
Baada ya salamu na utambulisho, mzee huyo alianza kwa kukiri kwamba kweli yeye ni baba mzazi wa Nasibu (Diamond) na kuweka wazi kwamba aliachana na mama mzazi wa msanii huyo miaka 9 iliyopita.
“Ni kweli mimi ndiye Abdul Juma, ni baba mzazi wa Nasibu au Diamond. Eee, mimi niliachana na mama Nasibu miaka tisa iliyopita, tena siku tunatengana niliondoka nyumbani saa tisa usiku, maana nilikuwa naishi kwao (ukweni).
AMGEUKIA DIAMOND
Kinyume na matarajio ya kuzungumzia mafanikio ya mwanaye kwa sasa, baada ya kuwekwa katikati na waandishi wetu, mzee Abdul ‘aliangusha’ kilio cha lawama kwa Diamond kuhusu matendo anayomfanyia kila kukicha.
Mzee huyo anayeonekana ‘kisharobaro’ alisema mafanikio makubwa aliyonayo mwanaye yasimfanye ashindwe kumthamini yeye kama baba na mapenzi yake kuyaelekeza kwa mama yake tu.
“Kuhusu Diamond, labda nimwambie huyu mtoto kuwa, amepata mafanikio ndiyo, lakini mafanikio hayo yasimfanye ashindwe kunithamini mimi kama baba yake na kupeleka mapenzi yote kwa mama yake tu,” alisema.
NI KWANINI?
“Nasema hivyo kwa sababu, zamani kabla jina lake halijawa kubwa, mawasiliano yetu yalikuwa mazuri sana, lakini nikaja kushangaa baada ya kuwa staa, akakata mawasiliano na mimi baba yake, aliangalie hilo.”
Akaongeza: “Sisemi kwa sababu nataka awe ananiletea hizo fedha zake, la hasha! Ila mimi kama baba yake ajue kuniheshimu.
“Diamond nampigia simu hapokei, namtumia meseji hajibu, maana yake nini? Naumizwa sana na kitendo cha kutopokea simu yangu kila ninapompigia kumjulia hali. Na hali hii ameanza mara baada ya kupata mafanikio.
JARIBIO LAIVU Katika kuthibitisha hilo, paparazi wetu alimtaka mzee huyo kumwendea hewani mwanaye ili kujiridhisha kama kweli ‘hapokeagi’ simu yake, simu ikapigwa, ikaita wee mpaka ikakatika.
Baba Diamond: “Si umeona, si nilikwambia ukawa huamini.”
MARA YA MWISHO KUMUONA DIAMOND
Mzee huyo aliendelea kutiririka kuwa, mara ya mwisho Diamond kufika nyumbani kwake ilikuwa mwezi wa tatu (Machi) mwaka huu baada ya hapo mawasiliano yakakatika.
“Diamond alikuja nyumbani kwangu mwezi wa tatu ikiwa ni mfungo wa tatu katika dini yetu ya Kiislam, akanipa fedha. Baada ya hapo hatujaonana tena wala hanijulii hali,” alilalama mzee wa watu.
SMS YA MWISHO KUIJIBU
Alisema Aprili, mwaka huu, Diamond alipotwaa tuzo tatu za Kili Music Awards 2012, yeye alimtumia ujumbe mfupi wa maneno akimpa hongera naye akajibu asante baba. Lakini baada ya hapo ikawa imetoka.
“Baada ya kufanikiwa kutwaa tuzo za Kili, mwaka huu nilimpigia simu mwanangu ili nimpongeze, hakupokea, nikamtumia SMS ndipo akajibu, ‘asante baba’, mchezo ukaishia hapo.
“Namshukuru sana dada yake, Mwajuma Abdul (Queen Darleen) yeye ndiyo yupo karibu sana na mimi kwani mara kwa mara anakuja kunitembelea na wakati mwingine hunikumbuka kwa fedha, hata pale aliposhinda tuzo ya Wimbo Bora wa Dancehall alifika nyumbani kunionesha tuzo yake, binafsi nilijisikia furaha,” alisema mzee Abdul ambaye kwa sasa hana mke.
HAJUI ANAPOISHI MWANAYE
Mbali na msanii huyo kutopokea simu ya baba yake kila anapompigia, vile vile mzee huyo alidai hajamuonesha wapi anapoishi.
“Huyu mtoto hajawahi kunionesha anapoishi, sijui anafikiri nikiwa karibu naye nitakuwa namuomba fedha. Mimi sina njaa ‘kihivyo’ na wala sitaki fedha zake, ila ninachotaka salamu tu, nasikiasikia anaishi Mwenge (usahihi ni Sinza Mori) lakini hataki kunionesha.
“Ninachojua yote haya yana mwisho kwani nyota aliyonayo sasa kuna siku itazima. Simuombei mabaya lakini inaniuma sana kunifanyia hivyo.”
DIAMOND APIGIWA SIMU MARA KUMI NA MBILI
Baada ya kupata matamshi hayo ya baba mzazi wa Diamond, mwandishi wetu siku ya Jumanne alifanya jitihada za kumpata msanii huyo ili ajibu ‘mashitaka’ hayo lakini licha ya kupigiwa simu mara kumi na mbili hakupokea.
Mbali na kupigiwa simu, paparazi wetu alimtumia ujumbe mfupi wa maneno kupitia simu yake ya mkononi, lakini pia hakujibu kitu. Juhudi za kumsaka zinaendelea.

Source: GPL

2 comments:

Comments system

Disqus Shortname